1 Mfalme Hezekia aliposikia haya, akararua nguo zake na kuvaa gunia, naye akaenda katika Hekalu la Mwenyezi Mungu. 2 Akawatuma Eliakimu msimamizi wa nyumba ya mfalme, Shebna mwandishi, na viongozi wa makuhani, wote wakiwa wamevaa magunia, waende kwa nabii Isaya mwana wa Amozi. 3 Wakamwambia, “Hili ndilo asemalo Hezekia: Siku hii ni siku ya dhiki, ya kukaripiwa na ya aibu, kama wakati watoto wanapofikia karibu kuzaliwa na kumbe hakuna nguvu ya kuwazaa. 4 Yamkini Mwenyezi Mungu, Mungu wako, atayasikia maneno ya jemadari wa jeshi, ambaye bwana wake, mfalme wa Ashuru, amemtuma kumdhihaki Mungu aliye hai, tena kwamba atamkemea kwa maneno ambayo Mwenyezi Mungu, Mungu wako, ameyasikia. Kwa hiyo omba kwa ajili ya mabaki ambao bado wako.”
5 Maafisa wa Mfalme Hezekia walipofika kwa Isaya, 6 Isaya akawaambia, “Mwambieni bwana wenu, ‘Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu: Usiogope kwa hayo uliyoyasikia, yale maneno ambayo watumishi wa mfalme wa Ashuru wamenitukana nayo. 7 Sikiliza! Nitatia roho fulani ndani yake, naye atakaposikia ujumbe fulani, atarudi nchi yake mwenyewe; nami huko nitafanya auawe kwa upanga.’ ”
8 Jemadari wa jeshi aliposikia kwamba mfalme wa Ashuru ameondoka Lakishi, alirudi, akamkuta mfalme akipigana na Libna.
9 Basi Senakeribu akapata taarifa kwamba Tirhaka Mkushi, mfalme wa Misri, alikuwa anaenda kupigana naye. Basi akatuma tena wajumbe kwa Hezekia na neno hili: 10 “Mwambieni Hezekia mfalme wa Yuda: Usikubali huyo Mungu unayemtumainia akudanganye wakati anaposema, ‘Yerusalemu haitatiwa mkononi mwa mfalme wa Ashuru.’ 11 Hakika umesikia yale ambayo wafalme wa Ashuru wametenda kwa nchi zote, wakiwaangamiza kabisa. Je, wewe utaokolewa? 12 Je, miungu ya mataifa ambayo yaliangamizwa na baba zangu iliweza kuwaokoa, hiyo miungu ya Gozani, Harani, Resefu, na ya watu wa Edeni waliokuwa Telasari? 13 Yuko wapi mfalme wa Hamathi, mfalme wa Arpadi, mfalme wa mji wa Sefarvaimu, au wa Hena au wa Iva?”
14 Hezekia akapokea barua kutoka kwa wale wajumbe, naye akaisoma. Kisha akapanda katika Hekalu la Mwenyezi Mungu, akaikunjua mbele za Mwenyezi Mungu. 15 Naye Hezekia akamwomba Mwenyezi Mungu akisema: “Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wa Israeli, unayeketi kwenye kiti cha enzi kati ya makerubi, wewe peke yako ndiwe Mungu juu ya falme zote za dunia. Wewe umeumba mbingu na nchi. 16 Tega sikio, Ee Mwenyezi Mungu, usikie; fungua macho yako, Ee Mwenyezi Mungu, uone; sikiliza maneno ambayo Senakeribu ametuma kumtukana Mungu aliye hai.
17 “Ni kweli, Ee Mwenyezi Mungu, kwamba wafalme wa Ashuru wameyaangamiza mataifa haya na nchi zao. 18 Wameitupa miungu yao kwenye moto na kuiangamiza, kwa kuwa haikuwa miungu, bali miti na mawe tu iliyotengenezwa kwa mikono ya wanadamu. 19 Sasa basi, Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wetu, tuokoe kutoka mkononi mwake, ili falme zote duniani zipate kujua kwamba wewe peke yako, Ee Mwenyezi Mungu, ndiwe Mungu pekee.”
20 Kisha Isaya mwana wa Amozi akapeleka ujumbe kwa Hezekia, akasema: “Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu, Mungu wa Israeli: Nimesikia maombi yako kuhusu Senakeribu mfalme wa Ashuru. 21 Hili ndilo neno ambalo Mwenyezi Mungu amelisema dhidi yake:
29 “Hii ndiyo itakuwa ishara kwako, ee Hezekia:
35 Usiku ule, malaika wa Mwenyezi Mungu akaenda, akawaua wanajeshi elfu mia moja na themanini na tano katika kambi ya Waashuru. Wenzao walipoamka asubuhi yake, walikuta maiti kila mahali! 36 Basi Senakeribu mfalme wa Ashuru akavunja kambi na kuondoka. Akarudi Ninawi na kukaa huko.
37 Siku moja, alipokuwa akiabudu katika hekalu la mungu wake Nisroki, wanawe Adrameleki na Shareza wakamuua kwa upanga, nao wakakimbilia nchi ya Ararati. Naye Esar-Hadoni mwanawe akawa mfalme baada yake.
<- 2 Wafalme 182 Wafalme 20 ->
Languages