Link to home pageLanguagesLink to all Bible versions on this site
Zaburi 101
Ahadi Ya Kuishi Kwa Uadilifu Na Kwa Haki
Zaburi ya Daudi.
1 Nitaimba juu ya upendo wako na haki yako;
kwako wewe, Ee Bwana, nitaimba sifa.
2 Nitazingatia kuishi maisha yasiyo na lawama:
utakuja kwangu lini?
 
Nitatembea nyumbani mwangu
kwa moyo usio na lawama.
3 Sitaweka mbele ya macho yangu
kitu kiovu.
 
Ninayachukia matendo ya watu wasio na imani;
hawatashikamana nami.
4 Moyo wa ukaidi utakuwa mbali nami;
nitajitenga na kila ubaya.
 
5 Kila amsingiziaye jirani yake kwa siri,
huyo nitamnyamazisha;
mwenye macho ya dharau na moyo wa kiburi
huyo sitamvumilia.
 
6 Macho yangu yatawaelekea waaminifu katika nchi,
ili waweze kuishi pamoja nami;
yeye ambaye moyo wake hauna lawama
atanitumikia.
 
7 Mdanganyifu hatakaa
nyumbani mwangu,
yeye asemaye kwa uongo
hatasimama mbele yangu.
 
8 Kila asubuhi nitawanyamazisha
waovu wote katika nchi;
nitamkatilia mbali kila mtenda mabaya
kutoka mji wa Bwana.

<- Zaburi 100Zaburi 102 ->
  • Zaburi